Daily Archives: September 29, 2021

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, tarehe 28 Septemba, 2021 amewapangia vituo vya kazi Mabalozi wafuatao:-

  1. Balozi Anisa Kapufi Mbega, Mkurugenzi wa Idara ya Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kuwa Balozi wa Tanzania nchini India.
  2. Balozi Innocent Eugene Shio, Kaimu Naibu Mkurugenzi wa Utawala Fedha na Mipango, Chuo cha Diplomasia-Dar es Salaam kuwa Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia.

Aidha, Mhe. Rais Samia pia amemhamisha kituo cha kazi Balozi Baraka Haran Luvanda kuwa Balozi wa Tanzania nchini Japan.

Kabla ya uhamisho huo Balozi Luvanda alikuwa Balozi wa Tanzania nchini India.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, tarehe 28 Septemba, 2021 amekutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia Dkt. Hafez Ghanem, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Rais Samia amemueleza Dkt. Ghanem vipaumbele vya Serikali ya Awamu ya Sita ambavyo ni kuboresha huduma za jamii ikiwemo elimu na afya pamoja na ujenzi wa miradi ya kimkakati.

Aidha, Mhe. Rais Samia amemueleza Dkt. Ghanem kuwa kwa sasa Serikali inapitia sera zake za kodi kwa majadiliano na wadau ili kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji katika kuimarisha sekta binafsi ili iweze kushindana na kuchangia ajira nchini.

Mhe. Rais Samia pia amezungumzia jitihada zinazofanywa na Serikali kuweka taarifa na kuongeza ufanisi katika makusanyo kupitia matumizi ya TEHAMA.

Kwa upande wake, Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia, Dkt. Ghanem amemshukuru Mhe. Rais Samia kwa kuendelea kushirikiana na Benki ya Dunia katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo nchini Tanzania.

Aidha, Dkt. Ghanem ameeleza dhamira ya Benki ya Dunia ya kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuwajengea uwezo wanawake kiuchumi kuanzia wanapozaliwa, kimasomo na katika afya.

Pia, Dkt. Ghanem amesema Benki hiyo ipo tayari kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika ununuzi, usafirishaji na utoaji elimu ya UVIKO 19 kwa jamii ili kutoa muamko kwa wananchi kujitokeza kupata chanjo.