Daily Archives: October 4, 2021

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, amesema kuwa katika kipindi chake cha uongozi atahakikisha anaimarisha chama cha Skauti nchini kutokana na kazi yake nzuri katika jamii ikiwemo kuunganisha vijana bila kujali dini, kabila, rangi, jinsia au itikadi ya kisiasa.

Mhe. Rais Samia amesema hayo tarehe 02 Oktoba, 2021 wakati akizungumza katika siku ya Mlezi wa  Skauti nchini iliyofanyika katika viwanja vya  Ikulu Chamwino mkoani Dodoma.

Aidha, Mhe. Rais Samia amekitaka Chama cha Skauti nchini, Girl Guides, na umoja wa vijana wa vyama vya siasa kuangalia suala la maadili kwa vijana na kutathmini mwenendo wao kwa kuwa licha ya kuwepo kwa mfumo mkubwa wa Taasisi hizo katika shughuli zake bado kumeendelea kuwepo na mmomonyoko wa maadili kwa vijana.

Pia, Mhe. Rais Samia amesema Chama cha Skauti kimesaidia kuitangaza nchi katika mikutano mbalimbali ambayo wamekuwa wakishiriki au kuindaa, mathalami Mkutano wa Skauti Kanda ya Afrika wa mwaka 2017 ambapo Chama cha Skauti Tanzania ilikuwa mwenyeji.

Mhe. Rais Samia amesema pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Chama cha Skauti nchini na mafanikio yaliyopatikana, Chama hicho bado kinakabiliwa na baadhi ya changamoto ikiwa ni pamoja na idadi ndogo ya wanachama na ukosefu wa fedha kwa ajili ya kuendesha shughuli zao.

Vilevile, Mhe. Rais Samia amewataka Viongozi na Wanachama wa Skauti kujikinga na kuwahamasisha wananchi wengine kuchukua tahadhari dhidi ya UVIKO 19, ikiwemo kupata chanjo na kushiriki kikamilifu kwenye zoezi la Sensa ya Watu na Makazi itakayofanyika mwezi Agosti 2022.

Mhe. Rais Samia amewataka Skauti nchini kushiriki kikamilifu katika kutangaza mafanikio yaliyopatikana  nchini katika kipindi cha miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara na miaka 59 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili Ulimwengu uweze kuyafahamu.

Katika hafla hiyo, Kamishna wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Salum Hamduni, amemkabidhi Mhe. Rais Samia Miongozo ya kuwawezesha na kuwafundisha vijana wa Skauti jinsi ya kuzuia na kupambana na rushwa.

Pia, Mhe. Rais Samia amewavisha Nishani Viongozi na watu mbalimbali waliochangia katika kuleta mafanikio ya Chama cha Skauti nchini.

Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan Ashiriki Maadhimisho Siku ya Mlezi wa Skauti Tanzania Mkoani Dodoma tarehe 02 Oktoba, 2021

Vijana wa Skauti wa Mkoa wa Simiyu Penina Mashimo kulia na Anastandhia Limbe kushoto, wakimvisha Skafu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mlezi wa Chama cha Skauti Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, alipowasili katika Viwanja vya Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma kwa ajili ya kuhudhuria katika Maadhimisho ya Siku ya Mlezi wa Skauti Tanzania.
.
Kamishna Mkuu wa Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa Nchini (TAKUKURU) Salum Hamduni akimkabidhi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mlezi wa Chama cha Skauti Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, Mwongozo wa kuwawezesha na kuwafundisha vijana wa Skauti jinsi ya kuzuia na kupambana na Rushwa Nchini, kwenye Maadhimisho ya Siku ya Mlezi wa Skauti Tanzania.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mlezi wa Chama cha Skauti Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akihutubia katika Maadhimisho ya Siku ya Mlezi wa Skauti Tanzania.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mlezi wa Chama cha Skauti Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akimvisha Tuzo Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mhe. Simai Mohammed Said, kwa kutambua mchango wake katika kuunga mkono Skauti Tanzania, kwenye Maadhimisho ya Siku ya Mlezi wa Skauti Tanzania.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mlezi wa Chama cha Skauti Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akimvisha Tuzo Kamishna Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini (TAKUKURU) Salum Hamduni kwa kutambua mchango wake katika kuunga mkono Skauti Tanzania, katika Maadhimisho ya Siku ya Mlezi wa Skauti Tanzania.
.