Daily Archives: September 17, 2023

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

RAIS SAMIA AHITIMISHA ZIARA YA KIKAZI MKOANI MTWARA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amewataka viongozi kuacha kuwanyonya wakulima kwa kuwakata fedha za mauzo na kuzipeleka katika mifuko ya maendeleo ambayo haipo kisheria.

Rais Samia ametoa tamko hilo wakati akihutubia katika mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa Bomani uliopo Masasi Mji.

Aidha, Rais Samia amewaelekeza viongozi hao kuiweka bayana mifuko iliyopo katika maeneo yao ili ijulikane, ikaguliwe na kuweka wazi mapato na matumizi yake.

Vile vile, Rais Samia amewataka watendaji wa Halmashauri ya Mji wa Masasi kuelekeza fedha za mapato ya halmashauri kutekeleza miradi ya maendeleo badala ya kusubiri fedha kutoka serikali kuu.

Kuhusu changamoto ya umeme katika Wilaya hiyo, Rais Samia amesema mkandarasi yuko kazini kuunganisha Masasi na gridi ya taifa na mradi huo unatarajiwa kukamilika baada ya miezi 18 hivyo kufanya umeme kuwa wa uhakika.

Awali Rais Samia alikagua ghala la kuhifadhi chakula la Mangaka wilayani Nanyumbu na kuzungumza na wananchi wa eneo la Round About ambapo amewaeleza kuwa Serikani inatarajia kujenga kongani ya viwanda wilayani humo.

Rais Samia amehitimisha ziara yake mkoani Mtwara na kuanza ziara katika mkoa wa Lindi ambapo amehutubia wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kata ya Likongolewe wilaya ya Liwale na Nachingwea mjini.

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

RAIS SAMIA AENDELEA NA ZIARA YA KIKAZI MKOANI MTWARA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amewataka viongozi katika ngazi zote kuwasikiliza wananchi na kujielekeza kwenye kutatua kero zao.

Rais Samia ametoa tamko hilo alipokuwa akizungumza na wananchi wa Newala katika uwanja wa Sabasaba mara baada ya kupokea taarifa za miradi ya maendeleo wilayani humo.

Akihutubia wananchi katika uwanja wa Majaliwa wilayani Tandahimba, Rais Samia amewaagiza Madiwani kusimamia vyema fedha za Halmashauri pamoja na fedha za miradi ya maendeleo zinazotolewa na Serikali ili waweze kuwahudumia wananchi.

Vile vile, Rais Samia ametaka viongozi wasimamie vizuri fedha za ruzuku zinazotolewa kwa wakulima ili ziweze kuzalisha zaidi.  

Rais Samia pia amewataka viongozi wa vyama vya ushirika kuhakikisha wanasimamia wakulima kupata pembejeo zinazotolewa na serikali ili kuepuka utolewaji wa takwimu za uongo na kuwanyima wakulima pembejeo hizo.

Rais Samia ameendelea na ziara yake mkoani Mtwara ambapo ameweka Jiwe la msingi jengo la utawala katika Halmashauri ya Wilaya ya Masasi.

Hali kadhalika, Rais Samia amezungumza na wananchi wa kijiji cha Nanguruwe wilaya ya Mtwara Vijijini pamoja na kusalimia wananchi wa kata ya Nanyamba.