Daily Archives: September 18, 2023

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

RAIS SAMIA AENDELEA NA ZIARA YAKE MKOANI LINDI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amesema serikali inatarajia kujenga kiwanda cha ukubwa wa kati cha kubangua korosho.

Rais Samia amesema hayo leo wakati akihutubia wananchi wa Ruangwa katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Kilimahewa.

Aidha, Rais Samia amesema lengo la kujenga kiwanda hicho ni kuwawezesha wananchi kuzalisha mafuta kwa kutumia maganda ya korosho ili waweze kupata faida zaidi na kuifanya Lindi ifunguke kiuchumi.

Vile vile, Rais Samia amesema serikali itaendeleza utafiti zaidi katika sekta ya madini ili kujua kiasi cha dhahabu kilichopo na kuwapanga wachimbaji wadogo wadogo ili wachimbe kitaalamu.  

Akizungumza na wananchi mara baada ya kuweka jiwe la msingi barabara ya Ruangwa – Nanganga (km 53.3) yenye thamani ya shilingi bilioni 50.3, Rais Samia amesema serikali ina mpango wa kuunganisha wilaya za mkoa wa Lindi kwa lami.

Mara baada ya kuweka Jiwe la Msingi kwenye ujenzi wa jengo la Halmashauri ya Mtama, Rais Samia amezungumza na wananchi na kuwataka kuongeza uzalishaji wa mbaazi na ufuta.

Rais Samia amezungumza na wananchi wa vijiji vya Nanganga na Nandagala akiwa njiani kuelekea Lindi mjini.