Daily Archives: November 2, 2023

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

TANZANIA NA UJERUMANI KUENDELEZA USHIRIKIANO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amesema serikali za Tanzania na Ujerumani zimekubaliana kuwa na mazungumzo ya ushirikiano wa maendeleo yatakayofanyika mwaka 2024.

Serikali hizo zimeagiza timu za wataalam kutoka pande zote mbili kuendelea kuwa na mazungumzo ya mara kwa mara yanayolenga kuimarisha ushirikiano na kubainisha maeneo mapya yenye umuhimu kwa nchi zote.

Rais Samia amesema hayo leo, wakati akizungumza na Waandishi wa Habari mara baada ya kumpokea na kuzungumza na Rais wa Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani, Dkt. Frank Walter Stainmeier ambaye yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu.

Aidha, Rais Samia ameeleza kuwa Tanzania iko tayari kufungua majadiliano kuhusu yaliyopita kwenye historia ya Utawala wa Ujerumani nchini ambapo mojawapo ni urejeshaji wa mabaki yaliyopo kwenye makumbusho mbalimbali za Ujerumani kwa

familia zao.

Rais Samia amesema anatambua juhudi za pamoja zinazofanywa  na taasisi za Serikali hizo mbili zinazolenga kufanikisha azma hiyo ikiwemo pia kuwajengea uwezo wataalam na kuongeza uwezo wa makumbusho za Tanzania na Ujerumani.

Rais Samia pia ameishukuru Ujerumani kwa namna inavyounga mkono Tanzania kwenye miradi ya maendeleo hususan sekta za afya, maji, kilimo, elimu, utalii, utamaduni, michezo, ulinzi, maliasili, uhifadhi wa mazingira na udhibiti wa fedha.

Kuhusu uwekezaji, Rais Samia amesema viongozi wote wawili wamekubaliana na kusisitiza mchango muhimu wa biashara na uwekezaji katika kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan akutana na Kuzungumza na Rais wa Ujerumani Mhe. Frank-Walter Steinmeier, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 31 Oktoba, 2023

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa na Mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Frank- Walter Steinmeier mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 31 Oktoba, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Frank-Walter Steinmeier akisaini Kitabu cha Wageni mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 31 Oktoba, 2023. Pembeni yake ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Frank-Walter Steinmeier mara baada ya kuwasili Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 31 Oktoba, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiongoza ujumbe wa Tanzania kwenye mazungumzo Rasmi na Rais wa Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Frank-Walter Steinmeier, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 31 Oktoba, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani Mhe. Frank-Walter Steinmeier akiongoza ujumbe wa Nchi yake kwenye mazungumzo Rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan aliyeongoza ujumbe wa Tanzania Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 31 Oktoba, 2023.