TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

RAIS SAMIA AITAKA MAHAKAMA KUIMARISHA MIFUMO YA UTOAJI HAKI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ameiagiza Wizara ya Katiba na Sheria pamoja na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kushirikiana na Wizara za kisekta kuzifanyia marekebisho sheria zote zenye mizunguko inayochelewesha kesi na upatikanaji wa haki.

Rais Samia ametoa agizo hilo leo katika maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika viwanja vya Chinangali.

Aisha, Rais Samia amesema Sheria mbalimbali zimetoa nafasi ya usuluhishi katika Mabaraza ya Vijiji na Kata hivyo amewataka majaji na Mahakimu kutoa mafunzo kwa kutumia utaratibu wa usuluhishi wa migogoro.

Rais Samia amewaagiza wadau wote katika Sekta ya Sheria kupitia upya taratibu ambazo mashauri hupitia ili kuzifupisha kwa lengo la kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa haraka.

Vile vile, Rais Samia amesema anatarajia kuona Watanzania wanatambua kwamba kufikishana mahakamani sio jambo la lazima na badala yake usuluhishi iwe ndio njia ya kwanza kutumika.

Rais Samia pia amesema ni lazima mfumo wa utoaji haki unaochukua muda mrefu kutatua migogoro urekebishwe kwa kuwa ni hatari, huongeza gharama na kuathiri mazingira ya uwekezaji na biashara.

Kwa upande mwingine, Rais Samia ameitaka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwachukulia hatua watumishi ambao wanachafua sura na taswira ya muhimili wa Mahakama kwa vitendo viovu vya rushwa, kauli mbaya na hata vitendo vya udhalilishaji kwa wanawake, watoto na wenye uhitaji maalum.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *